tuwasiliane

Friday, January 1, 2016

FARID MUSSA AENDA HISPANIA KUFANYA MAJARIBIO YA KUCHEZA SOKA YA KULIPWA



WINGA machachari chipukizi wa kimataifa wa Tanzania, Farid Mussa Malik anayechezea klabu ya Azam FC, anatarajiwa kwenda Hispania kufanya majaribio ya kucheza soka ya kulipwa.

Farid ameiambia BIN ZUBEIRY SPORTS - ONLINE kwamba ataondoka mapema wiki ijayo kwenda katika klabu ya bingwa ya Slovenia, FC Olimpija Ljubljana ambako amepewa siku 10 za majaribio.

"Kwa mujibu wa ratiba niliyopewa, mimi nitakwenda kuungana na hiyo timu Hispania kwa ajili ya majaribio hayo, naomba Watanzania wenzangu waniombee dua ili nifanikiwe tuongeze idadi ya wachezaji wanaocheza Ulaya,"amesema Farid.

Maana yake, sasa Farid hatacheza michuano ya Kombe la Mapinduzi inayotarajiwa kuanza Jumapili visiwani Zanzibar. 

Na huyo atakuwa mchezaji wa pili wa kikosi cha kwanza cha Azam FC kukosekana katika Kombe la Mapinduzi, baada ya beki wa kati, Aggrey Morris, ambaye anatarajiwa kwenda Afrika Kusini kufanyiwa upasuaji wa goti.
Mabingwa wa Afrika Mashariki na Kati, Azam FC, wanatarajiwa kuondoka leo jioni mjini Dar es Salaam kwa usafiri wa boti kuelekea visiwani Zanzibar kushiriki michuano ya Kombe la Mapinduzi.

Azam FC imepania kulitwaa tena taji hilo ambalo ilibeba mara ya mwisho mwaka 2012 wakiifunga Tusker FC ya Kenya katika fainali mabao 2-1 Uwanja wa Amaan, Zanzibar.

Azam FC itatupa kete yake ya kwanza Jumapili kwa kumenyana na mabingwa wengine wa zamani wa Kombe hilo, Mtibwa Sugar usiku, mchezio utatanguliwa na mchezo mwingine wa Kundi B kati ya mabingwa wa Tanzania Bara, Yanga SC dhidi ya wenyeji, Mafunzo ya Zanzibar.


No comments:

Post a Comment