tuwasiliane

Saturday, February 1, 2014

SIMBA YAITUNGUA JKT OLJORO,4-0

Na Mahmoud Zubeiry, Dar es Salaam
SIMBA SC imefufua matumaini ya ubingwa, baada ya leo kuifunga JKT Oljoro ya Arusha mabao 4-0 katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Ushindi huo, unaifanya Simba SC itemize pointi 30 baada ya kucheza mechi 15, ikiwa nafasi ya nne nyuma ya Mbeya City pointi 31, Yanga SC pointi 32 na Azam FC pointi 33 kileleni. 
Hadi mapumziko tayari Wekundu wa Msimbazi walikuwa mbele kwa mabao 3-0, matatu akifunga Mrundi Amisi Tambwe na moja kiungo mzalendo, Jonas Mkude.
Nyamazeni; Tambwe akishangilia bao lake la pili leo

Mabao yote hayo yalitokana na pasi na kiungo machachari wa pembeni wa timu hiyo, Ramadhani Yahya Singano ‘Messi’ ambaye kwa hakika alikuwa mwiba kwa safu ya ulinzi ya timu hiyo ya Jeshi la Kujenga Taifa. 
Jonas Mkude alifunga kwa shuti kali la umbali wa mita 20 baada ya kuletewa kwenye himaya yake moja kwa moja mpira wa kona uliopigwa na Messi.
Wachezaji wa Oljoro walijazana kwenye lango lao kumlinda kipa wao Mohamed Ali, lakini Messi akautoa nje kabisa mpira alipokuwa Mkude, ambaye aliunganisha moja kwa moja kwa shuti kali.
La kwanza; Jonas Mkude kulia akishangilia baada ya kufunga bao la kwanza
Tambwe akipongezwa na Awadh Juma kulia na Donald Mosoti kushoto
Haroun Chanongo akimuacha chini beki wa JKT Oljoro

Tambwe alifunga bao lake la kwanza leo na la pili kwa Simba SC dakika ya 22 akiunganisha krosi nzuri ya Messi wakati la tatu, alifunga dakika ya 28 baada ya kupata pasi ya kutanguliziwa kutoka kwa winga huyo machachari anayetumia vyema mguu wake wa kushoto.
Kipindi cha pili, Simba SC walirudi na moto wao na kufanikiwa kupata bao la nne dakika ya 52 mfungaji Tambwe tena, safari hii akiunganisha krosi ya Awadh Juma.
Baada ya mabao hayo manne, kocha Mcroatia akawapumzisha wachezaji wake nyota Messi, Amri Kiemba na Tambwe na kuingiza wachezaji wa kwenda kuulinda ushindi huo. 
Kikosi cha Simba SC leo kilikuwa; Ivo Mapunda, William Lucian ‘Gallas’, Issa Rashid ‘Baba Ubaya’, Donald Mosoti, Joseph Owino, Jonas Mkude, Haroun Chanongo, Awadh Juma, Amri Kiemba/Uhuru Suleiman dk64, Amisi Tambwe/Abdulhalim Humud na Ramadhani Singano ‘Messi’/Said Ndemla dk55.
JKT Oljoro; Mohamed Ali, Paul Malipesa, Ali, Omar, Nurdin Mohamed, Sabri Makame, Babu Ally, Jacob Masawe, Amir Omar, Shijja Mkina na Majaliwa Mbaga/Shaibu Nayopa dk38.

No comments:

Post a Comment