tuwasiliane

Monday, January 9, 2017

Jurgen Klopp: Sikukosea kuchagua kikosi cha Liverpool FA

Jurgen Klopp
Meneja wa Liverpool Jurgen Klopp ametetea uamuzi wake wa kuchezesha kikosi cha umri mdogo zaidi katika klabu hiyo kucheza mechi ya Kombe ya FA ambayo walitoka sare 0-0 na Plymouth.
Klabu hiyo sasa inalazimika kusafiri Devon kwa mchezo wa marudiano.
Huu ni mzigo ikizingatiwa kwamba klabu hiyo sasa itatakiwa kucheza mechi sita Januari.
Reds watakutana na Southampton kwenye mechi mbili nusufainali ya Kombe la EFL na wana mechi za Ligi ya Premia dhidi ya Manchester United, Swansea na Chelsea.
Hata hivyo, mkufunzi huyo kutoka Ujerumani alisema hafikiri kwamba alikosea kwenye uamuzi wake.
Wachezaji waliochezeshwa Jumapili walikuwa na umri wa kadiri wa miaka 21 na siku 296.
Mshambuliaji Ben Woodburn, 17, ndiye mfungaji mabao wa umri mdogo zaidi Liverpool baada yake kuifunga Leeds Kombe la EFL mapema msimu huu, na ni miongoni mwa waliokuwa kikosini.
Trent Alexander-Arnold, 18, na wachezaji watatu wa miaka 19 - Joe Gomez, Ovie Ejaria na Sheyi Ojo pia walichezeshwa.
Lucas, 29, ndiye mchezaji wa umri mkubwa zaidi wa Liverpool aliyechezeshwa.
"Ninawajibika, hata kama mnataka kulitazama kwa njia mbaya," alisema Klopp.
"Huwa nachagua kikosi cha kushinda mechi. Hatukufikiria kuhusu umri. Wete ni wachezaji muhimu katika kikosi chetu."
Daniel Sturridge, Adam Lallana na Roberto Firmino waliingizwa kipindi cha pili lakini Liverpool bado hawakufunga licha ya kudhibiti sana mpira.
"Tungelifanya vyema zaidi, 100%. Kipindi cha kwanza tulipoteza subira haraka, tukatoa krosi wakati usiofaa, tukatoa pasi zisizo sahihi.
"Tulikuwa na mpira wakati wote. Haikuvutia, haikuwa mechi ya kusisimua."
Plymouth, wanashikilia nafari ya pili kwenye Ligi ya Daraja la Pili.

No comments:

Post a Comment