tuwasiliane

Tuesday, December 13, 2016

Riyad Mahrez ashinda tuzo ya BBC ya mchezaji bora Afrika

Mahrez na kocha wake Leicester Claudio Ranieri
Riyad Mahrez ametawazwa kuwa Mwanakandanda Bora wa Afrika wa BBC wa Mwaka 2016.
Mashabiki kutoka kila pembe ya dunia walimpigia kura nyingi kiungo huyu wa kati wa Algeria na Leicester kuliko Pierre-Emerick Aubameyang, Andre Ayew, Sadio Mane na Yaya Toure.
Mahrez ameambia BBC Sport: "Naam, [tuzo hii] ina maana kubwa sana kwa sababu bila shaka mimi ni Mwafrika na ni jambo kuu sana kwa mchezaji wa Afrika nafikiri, kwa hivyo nina furaha isiyo na kifani, najivunia kuipokea.."
Tuzo hii ni kilele kwenye mwaka mzuri kwa mchezaji huyu wa miaka 25, ambaye tayari amejishindia taji la Ligi ya Premia na alishinda Tuzo ya Mchezaji Bora wa Mwaka chaguo la Wachezaji Uingereza.
Mahrez ametambuliwa kwa uchezaji wake mzuri kama mchawi katika wingi, ambaye familia yake inatoka kijiji kidogo kwa jina El Khemis nchini Algeria, ambaye alitikisa Ligi ya Premia.
Alisaidia sana Leicester City kushinda ligi bila kutarajiwa, ambapo alifunga mabao 17 na kusaidia ufungaji wa mabao 11 kuwawezesha kushinda, licha ya uwezekano wao kushinda mwanzoni mwa msimu kuwa 5000-1 pekee.
Mwezi Mei, Mahrez aliibuka Mwafrika wa kwanza kuteuliwa mchezaji bora zaidi ligini na wachezaji wenzake, miaka miwili tu baada yake kujiunga na Leicester kutoka Le Havre kwa £400,000.
Ni ufanisi mkubwa kwa mchezaji huyu aliyeanza maisha akicheza soka katika barabara za mtaa alipokuwa mtoto ambaye sasa amekuwa nyota anayeshindana na wachezaji bora zaidi duniani katika Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya.
Amefunga mabao manne katika mechi tano alizocheza Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya, ishara kwamba anaweza kutamba hati katika ligi zenye ushindani mkubwa zaidi

Katika mechi tano alizochezea Algeria, amefunga mabao mawili na kusaidia ufungaji wa magoli matano, na akawezesha Mbweha hao wa Jangwani kufuzu kwa mfainali za Kombe la Taifa Bingwa Afrika mwezi ujao.Kadhalika, ufanisi wake umetambuliwa na shirikisho la soka duniani FIFA, ambao walimuorodhesha kwenye orodha ya wachezaji watakaoshindania tuzo ya Mchezaji Bora wa Mwaka Duniani - Mwafrika pekee katika orodha ya wachezaji 23.
Mahrez sasa anajiunga na vigogo wa soka Afrika , wakiwemo Abedi Pele, Jay-Jay Okocha na Didier Drogba, ambao wamewahi kushinda Tuzo ya BBC ya Mwanakandanda Bora wa Afrika wa Mwaka.
Na ikizingatiwa kwamba bado ana miaka mingi ya kucheza, bado kuna muda kwake Mahrez kuwafurahisha mashabiki, ambao wameonesha jinsi wanavyompenda.

No comments:

Post a Comment