tuwasiliane

Sunday, September 14, 2014

UMBULULA,NA DHARAU KUIGHARIMU YANGA MIL 500

http://www.mwananchi.co.tz/image/view/-/2451198/highRes/642457/-/maxw/600/-/44ogfu/-/manji.jpg Klabu ya Yanga ipo hatarini kupoteza mamilioni ya fedha kama fidia kutokana na kutothamini, kutoheshimu mikataba baina yake na wadau mbalimbali wa soka ndani na nje ya nchi.


Uchunguzi wa gazeti hili unaonyesha  kuwa mabingwa hao wa kihistoria wa soka nchini wanaweza kulazimika kulipa fidia ya zaidi ya Sh500 milioni kama watabainika wamekiuka mikataba yao na Benki ya Posta, Emmanuel Okwi pamoja na klabu ya FC Lupopo.
Uongozi wa klabu hiyo  leo unalazimika kuwasilisha ushahidi  mbele  ya Kamati ya Sheria na Hadhi ya Wachezaji ya Shirikisho la Soka Tanzania kabla ya kamati hiyo kuiamuru kumlipa Okwi dola 50,000 (Sh81.1 milioni) anazoidai klabu hiyo.
Mwishoni mwa wiki iliyopita, kamati hiyo ya  TFF, chini ya mwanasheria Richard Sinamtwa ilimtangaza Okwi kuwa mchezaji huru baada ya Yanga kushindwa kutimiza matakwa ya mkataba.
Kutokana na hali hiyo, Yanga italazimika kumlipa Okwi mishahara yake ya miezi sita  sanjari  na Sh81.1 milioni za usajili. Okwi alikuwa kwa mwezi akipokea Sh4 milioni na kama kamati hiyo ya sheria itaamuru Yanga kumlipa mshahara wake wote, basi italazimika kumpa Sh24 milioni.
Mbali na Okwi, Yanga pia imejikuta ikiingia kwenye mgogoro na timu ya FC Lupopo ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC),  ambayo inaidai klabu hiyo dola 15,000 ( Sh24.7 milioni).
Viongozi wa FC Lupopo wamewasilisha barua  TFF kuomba msaada ili walipwe fedha zao ambazo ni za usajili wa beki Mbuyu Twite aliyetua  Yanga akitokea APR ya Rwanda, huku Lupopo ikidai klabu hiyo ya Twiga/ Jangwani kuwazunguka.
Kwa mujibu wa aliyekuwa ofisa habari wa TFF, Boniface Wambura (sasa Mkurugenzi wa Mashindano),  shirikisho hilo linayo barua ya Lupopo na katika makubaliano ya Yanga na Lupopo, kuna kipengele ambacho  kinailazimisha Yanga kuwapa sehemu ya asilimia ya fedha za usajili wa Twite.
Yanga kwa upande wake iliwalipa Lupopo dola 20,000 baada ya kumsajili Twite kwa mkataba wa miaka miwili uliomalizika msimu uliopita na tayari beki huyo  amesaini mkataba mwingine wa mwaka mmoja na hivyo timu hiyo ya Jangwani walipaswa kuwalipa  Lupopo dola 15,000, kama mkataba unavyosema, lakini jambo hilo halijafanyika.
Pia, Yanga imeingia kwenye mgogoro wa kimkataba na Benki ya Posta ambao walikubaliana kutengeneza kadi maalumu kwa ajili ya wanachama, lakini hivi karibuni Yanga walisaini mkataba kama huo na benki ya CRDB.
Meneja Uhusiano wa TPB, Noves Moses akizungumza siku moja baada ya Yanga na CRDB kusaini mkataba huo alisema: “Yanga walituletea notisi asubuhi ya kueleza nia yao ya kutoendelea nasi, lakini baadaye tukasikia kupitia vyombo vya habari wameingia mkataba na CRDB. 
“Kwa ufupi, Yanga hawakufuata utaratibu kwa vile walipaswa kutupa notisi ya miezi mitatu, lakini wao wametupa asubuhi na siku hiyo hiyo wameingia mkataba na CRDB, kama kuna upungufu tungeweza kujadiliana ni lazima sheria ichukue  mkondo wake,” alisema.


Kundi lingine linaloidai Yanga ni waliokuwa watendaji wake; aliyekuwa katibu mkuu wake, Celestine Mwesigwa na Louis Sendeu aliyekuwa ofisa habari.
Septemba mwaka jana, watendaji hao waliondolewa katika ajira zao kwa kile kilichoelezwa kuwa uongozi haukuridhika na utendaji wao.
Mwesigwa na Sendeu waliomba bila mafanikio walipwe na Yanga fidia ya Sh 262 milioni ambapo kati ya hizo, Sendeu anadai Sh79 milioni na Mwesigwa, Sh 183 milioni.

No comments:

Post a Comment