tuwasiliane

Thursday, June 19, 2014

Kiasi kingine kikubwa cha gesi chagunduliwa nchini


Kampuni ya Statoil ya Norway na mshirika wake ExxonMobil wamegundua kiasi kingine kikubwa cha gesi katika Bahari ya Hindi nchini Tanzania.
Kiwango hicho kinakadiriwa kufikia futi za ujazo trilioni mbili mpaka tatu (sawa na lita trilioni 56.6 hadi trilioni 84.9).
Ugunduzi huu unafanya jumla ya ujazo wa gesi iliyogunduliwa na washirika hao kufikia takriban futi za ujazo trilioni 20 (lita trilioni 566.25) kwenye Kitalu Namba 2, ambako washirika hao wanafanya shughuli za utafiti na uchimbaji.
‘’Tangu mwaka 2012 tumekuwa tukipata mafanikio ya asilimia 100 nchini Tanzania na eneo hilo limekuwa kitovu cha utafiti ndani ya muda mfupi. Ni kwa haraka tulitoka kwenye kuchimba kisima kimoja hadi kuwa na mkakati wa kuchimba visima vingi,’’ alisema Makamu wa Rais wa Shughuli za Utafiti za Statoil Ukanda wa Magharibi, Nick Maden.
Ugunduzi huo mpya katika Kisima Piri-1 umefanyika katika eneo lenye kiwango kidogo cha mawe ya mchanga kama ilivyokuwa wakati ilipogunduliwa gesi katika Kisima cha Zafarani-1 mwaka 2012.
Ugunduzi katika kisima hicho unakuwa wa sita katika Kitalu Namba 2.
Uchimbaji wa gesi katika kisima hicho ulifanywa na meli ya Discoverer Americas, usawa wa mita 2,360 za kina cha maji. Meli hiyo sasa inachimba kisima kingine cha Binzari katika Kitalu namba 2.
“Eneo lingine la utafiti limeshaandaliwa na litajaribiwa ndani ya mwaka 2014 na 2015. Tunatarajia kuchimba visima zaidi na tunatumaini kuwa matokeo ya visima hivi yataongeza kiasi cha ujazo wa gesi kwa ajili ya miundombinu ya mradi mkubwa wa gesi hapo baadaye,’’ alisema Maden.
Statoil ambayo imekuwapo nchini tangu 2007, inatafiti na kuchimba gesi katika kitalu namba mbili kwa niaba ya Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) ikiwa na hisa ya asilimia 65 katika kitalu hicho wakati ExxonMobil Exploration and Production Tanzania Limited ina asilimia 35.
SOURCE.www.mwananchi.co.tz

No comments:

Post a Comment