tuwasiliane

Saturday, January 11, 2014

Kapombe akimbilia Fifa, agoma kurudi Ufaransa

 
WAKALA wa Shomari Kapombe, Dennis Kadito amesema mchezaji huyo anaweza kupata uhalali wa kucheza timu yoyote ya Tanzania, lakini anatakiwa asubiri uamuzi wa kesi iliyofunguliwa Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa).
Kapombe amegoma kurudi Ufaransa kwenye timu yake ya AS Cannes.
Rafiki wa karibu wa beki huyo ambaye ni kiongozi mkubwa wa Simba ameiambia Mwanaspoti kuwa Kapombe kafikia uamuzi huo baada ya AS Cannes kushindwa kumlipa mshahara na kwa muda sasa wamekuwa wakimlipa nusu mshahara kiasi ambacho hakimtoshi kwa matumizi.
Kwa upande wake, Kadito amesema wamefungua kesi Fifa wakipinga uamuzi wa Cannes kushinikiza Shirikisho la Soka la Tanzania (TFF) limlipe Kapombe mshahara kwa muda wote aliokuwa nchini.
Lakini, Mwanaspoti linajua kuwa hata vibali vya kuishi nchini humo vimekuwa tatizo kwa Kapombe kitu ambacho kimemfanya ajisikie kama asiyethaminiwa.
Habari za ndani zinadai sababu nyingine ya Kapombe kugoma ni baada ya klabu yake kuamua kuwa TFF ndio watakaomlipa mshahara kwa kipindi chote alichobaki hapa nchini baada ya kuja kuichezea Taifa Stars dhidi ya Zimbabwe mwishoni mwa mwaka jana, katika mchezo wa kirafiki ambao Stars ililala kwa bao 1-0.
Wakala Kadito
“Ni kweli kuna matatizo hayo, kwa muda mrefu Kapombe amekuwa akilipwa nusu mshahara, alivyofika huku alikuwa hana akaunti, uongozi wa timu ulisema hautaweza kumlipa fedha zote anazotakiwa kulipwa bila ya kuwa na akaunti ambayo pia isingeweza kupatikana mpaka angepata viza ya kudumu ambayo ilikuwa ikihangaikiwa.
“Ilichukua muda mpaka kupatikana kwake na aliipata Novemba mwaka jana, mwezi huo alilipwa mshahara mzima lakini fedha alizokuwa akilipwa nusu ndiyo Cannes walikuwa wakishughulikia kuona wanamlipa na wakati huohuo ndio alikuja huko Tanzania,” alisema Kadito ambaye yupo Uholanzi.
Matatizo ya TFF
“Kulikuwa na matatizo yaliyosababishwa na TFF iliyopita, kwanza walimpatia tiketi ya ndege yenye matatizo, kutoka Tanzania mpaka Paris, Ufaransa kitu ambacho hakikuwa sahihi wakati kulikuwa na uwezekano wa kumtafutia ile ya moja kwa moja mpaka Cannes yalipo makazi ya timu. Niliwaambia kama watamleta Kapombe Tanzania kwa viza ambayo alikuwa akiitumia awali anaweza kupata shida wakati wa kurudi.
“Lakini wao wakafanya mipango yao bila kunishirikisha, matokeo yake nilichowaambia awali ndicho kilichotokea, Kapombe alifika mpaka Nairobi, Kenya akianza safari ya kurudi Ufaransa lakini akakwama kutokana na matatizo hayo.
“Awali kocha Kim Poulsen alinieleza juu ya kumhitaji Kapombe, nikamwambia kwa kipindi kile hakuwa sawa sana, wamuache kwanza lakini hakuniamini akaona kama nafanya njama ya kumzuia nikishirikiana na Cannes, ilinibidi nimtumie picha ya kidole ambacho alikuwa akikiuguza ili ajiridhishe,”alisema Kadito.
“Nilimshauri Kapombe baada ya kuniambia hataweza kurudi tena Ufaransa mpaka ajue hatma ya fedha zake, nikamwambia kwamba ingekuwa busara angerudi kule kuendelea na timu wakati ambao wao wanahangaikia malipo yake, unajua Cannes hawajakataa kumlipa wanachokasirika wao ni kutokuwepo katika timu kwa Kapombe.
“Leo (jana Ijumaa) nimezungumza na AS Cannes wanalalamika wametumia gharama kubwa kumtibu Kapombe, lakini ameanza kupona bila ya kuitumikia klabu kitu ambacho kimewakera na sasa wanaangalia uwezekano wa kuvunja mkataba au kumuuza, wamesema hawana tatizo katika kumuuza, watanipa majibu kuanzia kesho (leo Jumamosi) juu ya kiasi watakachomuuza ila wapo wazi kwa biashara.”
“Uwezekano upo lakini kwanza tunatakiwa kusubiri kuona Fifa itaamua nini katika hilo, nilishafungua madai juu ya matatizo hayo kumbuka Cannes wanaweza kupoteza nafasi yao ya umiliki wa Kapombe kutokana na tatizo la kutomlipa malipo yake ya msingi,’’ alisema Kadito.
source; mwanaspoti.co.tz

No comments:

Post a Comment