tuwasiliane

Saturday, March 30, 2013

MAITI ZAIDI ZAFUKULIWA BAADA YA JENGO KUANGUKA

Takriban watu kumi na saba mpaka sasa wamethibitishwa kufariki baada ya jengo lenye ghorofa zaidi ya kumi kuporomoka mjini Dar es Salaam, Tanzania.
Waokozi wanaendelea na shughuli ya kuwatafuta na kuwaokoa manusura na wanasema kuwa hadi sasa watu kumi na watatu waliokuwa wamenaswa wameokolewa.
Zaidi ya wengine sitini wangali wamenaswa chini ya vifusi.

Shughuli ya ujenzi ilikuwa inaendelea kwenye jengo hilo wakati lilipoporomoka katikati mwa mji wa Dar es Salaam.
Miongoni mwa watu ambao wangali kupatikana ni wafanyakazi wa mjengo na watoto kutoka shule jirani ya mafunzo ya dini ya kiisilamu.

Kulingana na walioshuhudia ajali hiyo, watu walisikika wakipiga mayowe kutaka msaada.
"nilidhani lilikuwa tetemeko la ardhi, na kisha nikasikia mayowe,'' alisema shahidi mmoja.
Jengo hilo liko katikati mwa Dar es Salaam na liliporomoka saa tatu kasorobo asubuhi kwa saa za Afrika mashariki.
Mamia ya watu wanaaminika kuwa ndani ya jengo hilo huku wengine wakiwa nje wakati wa ajali hiyo . Hata hivyo idadi kamili ya watu hao bado haujulikani.
Viongozi wamiminika
Rais Jakaya Kikwete alifika katika eneo la tukio saa 6:45 mchana na alipata maelezo mafupi ya tukio hilo kutoka kwa Mkuu wa Mkoa, Said Meck Sadik na Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova.
Baada ya maelezo hayo, Rais Kikwete aliyetumia dakika tisa, alimwambia Mkuu wa Mkoa na Kamanda Kova: “…mmiliki na mhandisi lazima wakamatwe mara moja.”
Kikwete baadaye alitikisa kichwa kuonyesha masikitiko na kuondoka.
Viongozi wengine waliofika ni Makamu wa Rais, Dk Mohammed Gharib Bilal ambaye hata hivyo hakuzungumza lolote hata baada ya kupata taarifa kutoka kwa mkuu wa mkoa.
Naye aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN) ambaye sasa ni Katibu wa NEC, Siasa na Uhusiano wa Kimataifa wa CCM, Dk Asha-Rose Migiro alisema tukio hilo linaumiza na kusikitisha kwani limepoteza nguvu kazi ya taifa.
“Ni vigumu kupata maneno ambayo yatabeba uzito wa tukio hili lakini wajenzi wanatakiwa kuwa makini na ujenzi wao,” alisema Migiro.

Wananchi wajitokeza kuokoa
Mapema Wananchi waliojitokeza kwa kushirikiana na askari polisi na mgambo wa Jiji walioanza kuondoa kifusi cha mchanga kwa kutumia mikono kutokana na kutokuwapo kwa vifaa vya kuondolea kifusi hicho.
Ilipofika saa 4.30 ndipo trekta (kijiko) moja lilifika na kushirikiana na wananchi ingawa halikuweza kuhimili kazi hiyo nzito na kuhitajika trekta maalumu la kubeba na si kuzolea ili kunusuru uwezekano wa kuhatarisha uhai wa waliofukiwa na kifusi.
Naibu Meya wa Halmashauri ya Ilala, Kheri Kessy alisema,mwaka 2007 walitoa kibali kwa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kwa kushirikiana na ‘Ali Raza Investment Limited’ kujenga jengo la ghorofa 10.
“Kibali tulichotoa sisi ni cha kujenga ghorofa 10 na mkaguzi wetu alikuwa anafuatilia kila hatua hadi ilipofika ghorofa ya 10 akawa amemaliza kazi yake,” alisema Kessy.
Alipotakiwa kueleza kwanini hawakuchukua hatua baada ya kuendelea kujengwa hadi kufikia ghorofa zaidi ya 16 alisema, wao kwa hilo hawahusiki ila kuna taasisi zingine za Serikali zinazosimamia majengo zinatakiwa kuulizwa.
“Kama nilivyosema,sisi tulitoa kibali cha kujenga ghorofa 10 na mkaguzi wetu alikagua hadi ghorofa ya 10 hivyo kama waliendelea kujenga sisi hatujui kwani kuna CRB (Bodi ya Usajili wa Makandarasi) au ERB (Bodi ya Usajili ya Wahandisi) wao ndio wanahusika zaidi watawaelezeni,” alisema Kessy.
NHC yatoa maelezo
Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) jana lilitoa taarifa yake kuhusu tukio hilo na kueleza kuwa mradi wa ujenzi wa ghorofa hilo ulikuwa ukifanyika kwa ubia kati yake na Kampuni ya Ujenzi ya Ladha ya jijini Dar es Salaam, ambapo NHC lilikuwa na ubia wa asilimia 25.
Ilieleza kuwa mbia huyo alipaswa kabla ya kuanza ujenzi kupata vibali kutoka kwenye mamlaka husika na kuwa na wataalam wa ujenzi na washauri  waliokubalika na kuthibitishwa na mamlaka husika, kwani NHC ilitoa ardhi tu kwa ajili ya ujenzi huo na ubia ungekamilika mara baada ya jengo hilo kumalizika kujengwa.
“Mbia akishapata wataalam hao yeye ndio  anayehusika kuingia nao mikataba ya kazi ya kujenga na kusimamia ubora wa jengo husika kwa mujibu wa sheria” ilieleza taarifa hiyo.
Ilieleza kuwa NHC imesimamisha utoaji wa miradi mipya ya ubia ili kuweza kutathimini mafanikio na changamoto za utekelezaji wa miradi ya ubia na hivyo kuwezesha kutengeneza sera mpya.

No comments:

Post a Comment