tuwasiliane

Tuesday, December 27, 2011

27 DEC. PAPIC MBIONI KUITEMA YANGA


'NDOA' ya Kocha Kostadin Papic na klabu ya Yanga ya jijini Dar es Salaam, haijasimama kwenye mstari ulionyoka na kwa sababu hiyo, huenda akaachia ngazi kama uongozi hautarekebisha kasoro zilizopo.Jana, Papic aliyerejea kuifundisha Yanga kwa mara ya pili, alikutana na waandishi wa habari na kueleza wazi jinsi mambo yalivyo magumu Jangwani.

Katika mengi aliyoeleza mbele ya waandishi, msingi mkuu wa malalamiko yake ni kutengwa kiushirikiano na viongozi wa Yanga.Papic alisema hapati ushirikiano wa kutosha toka kwa viongozi wa klabu hiyo pamoja na jitihada kubwa ya kufanya nao mawasiliano.

"Ni kama wamenitenga, hatuwasiliani kama inavyopaswa kuwa, napiga simu zao hawapokea na wakati mwingine hazipatikani."Unafanya vipi kazi na watu wasiokuwa ushirikiano hasa katika kipindi hiki timu inakabiliwa na michuano ya kimataifa," alisema.

"Klabu ina hali mbaya kifedha, mimi na wachezaji hatujalipwa mishahara yetu mpaka leo na uongozi umekaa kimya bila kusema lolote," alilalama Papic.Alisema wachezaji wake wamekaa kimya lakini haina maana kwamba wanafurahishwa na hali ya mambo ndani ya klabu.

"Wachezaji wangu hawajasema lolote, lakini kwa kuwangalia wanaonekana kuumia na hali hii ya kutolipwa mshahara mpaka sasa. Sura zao matumaini zimepotea kabisa."

Alisema anashangazwa na ukimya wa uongozi wa Yanga katika kipindi ambacho wanakabiliwa na mtihani mgumu wa mechi ya Ligi ya Mabingwa dhidi ya Zamalek.

Papic aliyewahi kufundisha soka nchi kadhaa Afrika, alisema katika mazingira magumu kama hiyo si rahisi kuwaandaa wachezaji kupata ushindi."Siyo kwamba najitetea, lakini kama timu itashindwa kufanya vizuri kwenye mechi hiyo, basi asilaumiwe yeye wala wachezaji wake."
"Hatujafanya mazoezi kwa siku saba ukiacha siku tatu za mvua. Mbali na mazoezi ya uwanjani hata Gym hatujakwenda.

"Nimechukua jukumu la kuwakumbusha mara kwa mara viongozi kushughulikia suala hili, lakini mpaka leo sijapata jibu la maana.Papic amesema amekata tamaa ya kufanya vizuri kwenye mechi hiyo kwa vile uongozi wake umesema wazi hauna pesa."Hakuna mazoezi, hakuna mechi za kirafiki ukiuliza unaambiwa wiki ijayo, kila siku wiki ijayo, hakuna kinachotekelezwa.

"Nimeomba mechi sita za kirafiki za kimataifa lakini hakuna kinachotekelezwa mashabiki wasije kuwalaumu wachezaji kwa lolote hali halisi ndio hiyo.Kuhusu mkataba wake na Yanga, Papic alilalamika kutothaminiwa, akitoa mfano wa kuishi kwenye mazingira magumu baada ya nyumba aliyopangishiwa kukatwa maji na umeme.

"Hali ni ngumu kwangu binafsi na kwa wachezaji wangu, kuamua kwangu kuzungumza ni kwa sababu hali imefika hatua ambayo haipaswi kuvumiliwa."Kujiuzulu ni silaha yangu ya mwisho lakini kwanza napambana, kusaka wadhamini na wadau wa kutusaidia iwapo itashindikana sitakuwa na jinsi," alisisitiza.

"Yanga ina wanachama na mashabiki wengi, ni vizuri wakasikia kilio hiki na kujitokeza kusaidia ili timu ipate mahitaji na kujiandaa vizuri."

Akijibu malalamiko ya Papic, mmoja kati ya viongozi wa juu wa klabu hiyo ambaye hakutaka jina lake kuandikwa gazetini, alisema ameshangazwa na kauli za Papic kwa waandishi wa habari.

Alisema kimsingi Papic hakupaswa kuongelea matatizo ya wachezaji kwa vile si jukumu lake. "Ameita waandishi wa habari na kuwaeleza matatizo ya wachezaji, haitasaidia kwa sababu matatizo ya klabu yatamalizwa na klabu na si vyombo vya habari," alisema bosi huyo.

Kuhusu kutaka kujiuzulu, alisema: "Kama Papic anaona ipo sababu ya kufanya hivyo hatuwezi kumzuia kwa vile ana haki ya kuamua bila kushurutishwa."

Kiongozi huyo pia alishangazwa na kauli kwamba (Papic) hajalipwa mshahara mpaka leo. "Nimkumbushe kwamba, aliposaini mkataba na Yanga tulimpa mishahara ya miezi miwili mbele, leo anasemaje kwamba hajalipwa mshahara," alihoji.

Kuhusu suala la kukatiwa maji na umeme, alisema hilo ni jukumu lake. "Hivi ukikatiwa umeme na maji nyumbani kwako utakwenda ofisini kulalamika?"

Kuhusu wachezaji kutolipwa mishahara, alikiri ni kweli hawajalipwa kwa vile tarehe wanayolipwa bado haijafika.
"Mishahara ya wachezaji inalipwa tarehe 28 kila mwezi, sasa leo ni tarehe ngapi mtu afikie kusema wachezaji hawajalipwa mishahara," alihoji bosi huyo.

Kuhusu mazoezi, alisema anachofahamu yeye ni kwamba walisimama wakati wa mvua na si vinginevyo. "Anasema hawajaenda kufanya mazoezi Gym inashangaza kwa sababu klabu ina Gym.

Papic aliwahi kuinona Yanga toka Januari 2009 mpaka 2010 kabla ya kumwaga manyanga kwa madai ya kuingiliwa kiutendaji na uongozi wa Yanga.

Alirejeshwa tena kuchukua nafasi ya Kocha Sam Timbe raia wa Uganda aliyetimuliwa kwa madai ya kushindwa kuibadilisha timu ingawa aliiwezesha kutwaa taji la Ligi Kuu na Kombe la Kagame.

Kabla ya kutua Yanga pia aliwahi kufundisha timu za Orlando Pirates, Maritzburg United, Kaizer Chiefs na Hearts of Oak.

No comments:

Post a Comment