tuwasiliane

Thursday, January 12, 2017

KOCHA AZAM AAHIDI USHINDI DHIDI YA SIMBA KESHO USIKU

KUELEKEA fainali ya michuano ya Kombe la Mapinduzi keshokutwa Ijumaa, Kocha Msaidizi wa Klabu Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati Azam FC, Idd Nassor Cheche, ameweka wazi kuwa wanajua namna ya kuikabili Simba na kupata matokeo mazuri kwenye mchezo huo.
Cheche ametoa kauli hiyo kwenye mazoezi ya kwanza ya Azam FC jioni ya leo ya kujiandaa na mchezo huo, ambapo imeingia fainali baada ya kuichapa Taifa Jang’ombe bao 1-0, lililofungwa kwa shuti kali na kiungo Frank Domayo.
“Mchezo utakuwa mgumu, sisi tumewaona tokea mwanzo kwenye michuano hii na tunawajua tokea huko nyuma na mwalimu waliokuwa naye na sisi tulikuwa naye tunamjua na tunajua ni vitu gani tutafanya, hatuwezi kusema hivi sasa utakuja kuviona uwanjani wakati tunacheza kama tulivyowaahidia kwenye mechi na Yanga,” alisema Cheche wakati akizungumza na mtandao rasmi wa klabu hiyo www.azamfc.co.tz  
Alisema katika mazoezi ya kwanza wachezaji wa kikosi hicho wameyaanza vema wakiwa na furaha na mwanzo mpya huku akidai kuwa licha ya ushindani utakaoonyeshwa kwenye mchezo huo wamejipanga kukabiliana na hali hiyo.
Cheche ambaye atakiongoza kikosi hicho kama kocha mkuu hadi kumalizika kwa michuano hiyo kabla ya kumpisha Kocha Mkuu mpya wa Azam FC aliyetambulishwa jana, Aristica Cioaba raia wa Romania, mpaka sasa amekiongoza kikosi hicho kuandika rekodi ya aina yake ya kutofungwa mchezo wowote wala kuruhusu bao.
Hadi inaingia fainali kwa kuitoa Taifa ya Jang’ombe, Azam FC kwenye hatua ya makundi iliichapa Zimamoto bao 1-0, ikatoa suluhu na Jamhuri kabla ya kuifumua Yanga mabao 4-0, ukiwa ni ushindi wa kihistoria tokea timu hizo zianze kukutana.
Azam FC kesho Alhamisi jioni itamalizia mazoezi yake ya mwisho kabla ya kuivaa Simba kwenye mchezo wa fainali unaosubiriwa kwa hamu na mamilioni ya Watanzania wapenzi wa soka.

No comments:

Post a Comment