tuwasiliane

Saturday, December 26, 2015

YANGA VS MBEYA CITY KAZI IPO LEO TAIFA

Kocha wa Yanga Hans van der Pluijm (kulia) na Msaidizi wake Juma Mwambusi
Kocha Hans van der Pluijm wa Yanga  leo Jumamosi atakuwa na kazi ya kuhakikisha timu yake inaendelea kubaki kileleni mwa msimamo wa ligi ya Vodacom, wakati itakapo ikaribisha Mbeya C...
Katika mchezo uliopita wakiwa kwenye uwanja huo mabingwa hao watetezi waliibuka na ushindi mnono wa mabao 4-0 dhidi ya Stand United ya Shinyanga huku mshambuliaji wake Amissi Tambwe akifunga Hat- Trick yake ya tano ukiwa ni msimu wa tatu tangu alipoanza kucheza ligi ya Vodacom Tanzania bara.
Mbeya City haipewi nafasi kubwa ya kuwazuia Yanga kutokana na mwenendo wake wa kusuasua tangu ilipoanza msimu huu na kuondoka kwa kocha Juma Mwambusi ambaye amehamia Yanga ndiyo kumeongeza asilimia ya timu hiyo kupoteza pambano hilo.
Lakini mbali ya mwenendo mbaya wa Mbeya City, kikosi cha Yanga kwa sasa kimekuwa kwenye kiwango cha juu hasa safu yake ya ushambuliaji inayoongozwa na Mzimbabwe Donald Ngoma , ambaye katika mchezo uliopita dhidi ya United aliweza kutengeneza nafasi mbili za mabao yaliyofungwa na Tambwe.
Kocha Abduli Mingange aliyechukua nafasi ya Juma Mwambusi hatarajiwi kuwa na miujiza kwani hata kikosi chake hakina mchezaji mwenye uwezo wa kuiweza kuisumbua Yanga ikiacha kipa wake mkongwe Juma Kaseja aliyewahi kuichezea Simba.
Rekodi zinaonyesha Mbeya City, haijawahi kuifunga Yanga tangu ilipopanda kucheza ligi ya Vodacom misimu miwili iliyopita na katika mara mbili zilipokutana uwanja wa taifa timu hiyo ilipoteza mechi zote mbili na katika mechi mbili zilizochezwa uwanja wa sokoine mechi moya Yanga ilishinda mabao 3-1 na nyingine ilitoka sare ya kufungana mabao 1-1.
Kocha Juma Mwambusi pia atahusika katika kuiangamiza timu hiyo kwasababu anajua vizuri mapungufu waliyokuwa nayo na atakuwa na kazi nyepesi ya kumshauri boss wake Hans van der Pluijm, ili wapate ushindi ambao utaendelea kuwabakisha kileleni mwa ligi hiyo.
Awali kabla hajahamia Yanga Mwambusi aliwahi kukiri kuwa Yanga ndiyo timu kubwa ambayo ilikuwa ikiwasumbua nab ado alikuwa anaitafutia dawa kuhakikisha wanaifunga lakini hadi anaondoka timu hiyo hakuwa kupata ushindi mbele ya Yanga.
Mchezo wa mwisho Mbeya City ilicheza nyumbani uwanja wa Sokoine na kulazimishwa sare ya 1-1 na Mgambo JKT, hivyo niwazi pamoja na ubora wa Yanga lakini timu hiyo itakuja imejipanga kuhakikisha inapata ushindi wa ugenini ambao utawatoa kwenye nafasi ya 10 waliopo hivi sasa wakiwa na pointi zao 11.
Kocha Mingane katika dirisha dogo la usajili alimsajili beki wa Coastal Union Tumba Sued, kuziba pengo la nahodha wake Juma Nyosso, aliyefungiwa kwa miaka miwili mchezaji huyo anaweza kuwa msaada mkubwa katika mchezo wa Jumamosi kwa kuwazuia akina Ngoma na Tambwe.
Kocha wa Yanga Mholanzi Pluijm, naye huenda leo akawatumia kwa mara ya kwanza nyota wake wawili aliowasajili kwenye dirisha ldogo la usajili mshambuliaji Paul Nonga aliyewahi kuichezea Mbeya City na mwanzoni mwa msimu huu kuhamia Mwadui FC, na kiungo wa kimataifa kutoka Niger Boubakar Garba.
Wachezaji hao wamefanya mazoezi kwa asilimia 100 na kikosi cha Yanga na Pluijm, ameahidi kuwatumia ili kuanza kuitumikia timu hiyo ambayo kwasasa imekuwa na ushindani mkubwa na Azam FC, katika mbio za kuwania taji la Vodacom.

No comments:

Post a Comment