tuwasiliane

Wednesday, August 27, 2014

OKWI,BUTOYI OUT,


Rais wa Simba, Evans Aveva amemaliza utata wa usajili wa wachezaji wa kigeni uliokuwa umeigubika klabu hiyo kwa kusema Mkenya Donald Mosoti ndiye anabaki na Mrundi Butoyi Hussein wamempiga chini huku Yanga nao wakimpiga chini Emmanuel Okwi raia wa Uganda.

Simba na Yanga zimelazimika kufanya uamuzi mgumu wa kupunguza idadi ya wachezaji wa kigeni ambao wamezidi katika klabu zao kwa sababu usajili wa wachezaji katika klabu za Ligi Kuu Bara unamalizika leo saa 6 usiku.
Akizungumza na chanzo chetu, Aveva alisema kuwa Butoyi alikuja kwa ajili ya majaribio na si kusajiliwa hivyo mchezaji atakayebaki ni Mosoti ambaye bado ana mkataba na klabu hiyo.
“Mosoti ni mchezaji wetu na ndiye atakayebaki, sioni kama kuna sababu ya kufanya mabadiliko kwa sasa kwani hata kama kocha angekuwa anamhitaji Butoyi angekuwa ameshatuambia, huyo alikuja kwa ajili ya majaribio,” alisema Aveva.
Siku nzima ya jana viongozi wa Kamati ya Usajili ya Simba walikuwa na vikao visivyomalizika ili kuhakikisha wanakamilisha suala hilo, ambapo jana hiyo hiyo jioni walitakiwa kupeleka taarifa yao ya usajili katika kikao cha Kamati ya Utendaji.
Kikao hicho cha Kamati ya Utendaji kilitarajiwa kuongozwa na Aveva ili kufunga mjadala wa usajili wa wachezaji wao watakaoitumikia klabu hiyo msimu ujao.
Habari kutoka visiwani hapa, ambapo Simba imeweka kambi zinaeleza kwamba juzi Jumatatu usiku kocha Patrick Phiri alifanya kikao na benchi la ufundi na kuwashirikisha juu ya uamuzi wake na wote waliridhia kubaki kwa Mosoti.
Hata hivyo Phiri hakuwa tayari kuweka wazi juu ya suala hilo huku akisema, “Nimetuma taarifa kwa viongozi wangu juu ya mchezaji ninayemtaka, hivyo nasubiri majibu kutoka kwao, lakini sipendi kufanya mambo kwa kukurupuka, kila kitu kifanywe kwa utaratibu.
“Nina mapendekezo yangu, lakini kabla hayajatolewa uamuzi ni lazima yajadiliwe na viongozi ila lazima jibu lipatikane,” alisema Phiri.
Kwa kukatwa Butoyi, wachezaji watano wa kigeni waliobaki Simba ni Joseph Owino, Donald Mosoti, Amissi Tambwe, Pierre Kwizera na Raphael Kiongera.
Kwa upande wa Yanga ambayop nayo ilikuwa na wachezaji sita wa kigeni, jumba bovu limemwangukia, Emmanuel Okwi.

Kwa mujibu wa chanzo hicho cha habari ni kwamba, uwezo na nafasi wanazocheza wachezaji hao ni tofauti hivyo waliangalia mahitaji ya timu wapi kwenye upungufu ili mmoja wao abakie. Kiiza anajulikana ni mzuri zaidi anaposimama kati kama mshambuliaji na Okwi ni mzuri kucheza nyuma ya straika au pembeni.
Yanga hivi sasa ina wachezaji wengi wa viungo wenye uwezo wa kucheza winga kama, Andrey Coutinho, Simon Msuva, Haruna Niyonzima, Nizar Khalfan, Omega Seme, Hamis Thabit, Hassan Dilunga.
Tofauti na ilivyo kwa washambuliaji wa kati ambao ni Geilson Santos Santana ‘Jaja’, Said Bahanuzi, Jerry Tegete, Hussein Javu na Kiiza.
Awali Hamis Kiiza ambaye pia ni raia wa Uganda ndiye aliyekuwa anadaiwa kuachwa, lakini habari za ndani kutoka katika klabu ya Yanga zinasema jumba bovu limemwangukia Okwi ambaye hadi jana asubuhi alikuwa hajajiunga na timu.


No comments:

Post a Comment