tuwasiliane

Saturday, April 19, 2014

Mwaliko sherehe za ubingwa Azam leo

 
UONGOZI wa klabu ya Azam FC unawaalika wapenzi na wadau wa timu hiyo katika sherehe za ubingwa zitakazofanyika leo makao makuu ya klabu, Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam baada ya mchezo wake wa mwisho wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya JKT Ruvu.
Katibu wa Azam FC, Nassor Mohammed Idrissa ‘Father’ ameiambia tovuti ya klabu kwamba, katika sherehe hizo watu wote watakaokata tiketi za kuingia kutazama mchezo dhidi ya JKT Ruvu, watahusishwa moja kwa moja.

Aidha, Father amesema kwamba katika sherehe hizo wanaalikwa pia wadau wote wa Azam wakiwemo wachezaji wa zamani wa timu hiyo na wadau wengine wa soka nchini.
“Tunawaalika katika sherehe zetu za ubingwa wadau, wapenzi na wachezaji wa zamani wa Azam FC leo baada ya mechi yetu na JKT Ruvu, waje tujumuike tusherehekee, tule tunywe kwa furaha,”alisema Father.
Azam ilitwaa ubingwa wa Ligi Kuu Jumapili, baada ya kuifunga Mbeya City mabao 2-1 Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya, huku waliokuwa wapinzani wao katika mbio za taji hilo, Yanga SC wakishinda 2-1 dhidi ya JKT Oljoro mjini Arusha.

Azam imefikisha pointi 59 ikiwa na mchezo mmoja mkononi ambazo haziwezi kufikiwa na timu yoyote baada ya mechi za mwisho kesho, kwani Yanga SC yenye pointi 55 sasa ikiifunga Simba SC itafikisha 58.
Licha ya kuwa timu ya kwanza kuifunga Mbeya City kwenye Uwanja wake Aprili 13, mwaka huu, Azam FC pia inakuwa timu ya kwanza nje ya Simba na Yanga kutwaa ubingwa wa Bara tangu mwaka 2000 Mtibwa Sugar ilipofanya hivyo

Azam inakuwa timu ya saba nje ya Simba SC kutwaa taji la Ligi Kuu, baada ya Cosmo mwaka 1967, Mseto mwaka 1975, Pan Africans mwaka 1982, Tukuyu Stars mwaka 1986, Coastal Union 1988 na Mtibwa Sugar mara mbili mfululizo 1999 na 2000.

source. azamfc.co.tz

No comments:

Post a Comment