tuwasiliane

Saturday, June 8, 2013

TAIFA STARS KUFANYA KWELI LEO?

 


TAIFA STARS inacheza mechi ya pili ya mchujo ya Kombe la Dunia ugenini leo Jumamosi dhidi ya wenyeji Morocco ‘Lions of the Atlas’ huku ikipania kupata matokeo mazuri.
Mechi hiyo ya nne kwa Taifa Stars katika michuano hiyo hatua ya makundi inachezwa saa 3:00 usiku kwa saa za hapa, ambapo kwa Tanzania itakuwa saa 5:00 usiku kwenye Uwanja wa Grand Stade, mjini Marrakech.
Akizungumzia mechi hiyo, Kocha wa Stars, Kim Poulsen amesema timu yake inatarajia kucheza vizuri lengo likiwa ni kuhakikisha inapata matokeo baada ya dakika 90 za mechi hiyo itakayochezeshwa na Daniel Frazier Bennett kutoka Afrika Kusini.
“Unapocheza ugenini ni lazima uwe makini na mwangalifu. Usiruhusu mpinzani wako akakuvuruga hasa dakika 20 za mwanzo. Lengo letu kuja hapa ni kufanya vizuri, na tumejiandaa kimwili na kiakili,” alisema Kim ambaye ameiongoza Stars kushinda mechi mbili nyumbani dhidi ya Gambia na Morocco na kupoteza ugenini mbele ya Ivory Coast katika Kundi hilo la C.
Ubora wa Stars katika mechi hiyo ni katika kumiliki mpira na kutoa pasi zitakazowafanya kushambulia kwa urahisi wakati Morocco inategemea zaidi uwezo wa mchezaji mmoja mmoja na wengi wao wa kikosi cha kwanza wanacheza mpira wa kulipwa Ulaya.
Kwa upande wa maandalizi, Kim alisema Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager imejiandaa vizuri kwani ilikuwa na kambi ya wiki moja nyumbani, wiki moja nyingine ikapiga kambi nchini Ethiopia, na baadaye hapa Marrakech ambapo pia imekuwepo kwa wiki nzima ikijiwinda kwa mechi hiyo.
Ikiwa nchini Ethiopia ilicheza mechi ya kirafiki dhidi ya Sudan iliyomalizika kwa timu hizo kutoka suluhu huku Kim akiwapa fursa ya kucheza wachezaji 16 akiwemo Haruni Chanongo aliyecheza dakika kumi za mwisho, ikiwa mechi yake ya kwanza baada ya kuitwa katika kikosi hicho kwa mara ya kwanza.
Ndani ya miaka miwili, Stars itakuwa inakutana na Morocco kwa mara ya nne. Mwaka 2011 katika mechi za kutafuta tiketi ya Fainali za Kombe la Afrika mwaka 2012 nchini Afrika Kusini, Stars ilifungwa nje ndani (1-0 jijini Dar es Salaam na 3-1 jijini Marrakech).
Lakini katika mechi iliyopita Machi 24 mwaka huu Stars iliibuka na ushindi wa mabao 3-1,  yote yalifungwa kipindi cha pili. Shukrani kwa mabao hayo ya Mbwana Samata (mawili) na Thomas Ulimwengu.
Kim alisisitiza kuwa malengo yake kwa sasa ni kupigania nafasi ya kucheza Fainali za Kombe la Dunia na kwamba timu yake imekuwa ikifanya vizuri kadri inavyoendelea kucheza ikiwa imeshafunga mabao matano katika mechi hizo za mchujo.
“Tulianza safari kwa kufungwa 2-0 ugenini na Ivory Coast. Katika mechi ile hatukupata bao na tukamaliza tukiwa kumi uwanjani baada ya mchezaji wetu mmoja kutolewa kwa kadi nyekundu. Lakini kadri tunavyoendelea katika mashindano ndivyo timu inavyozidi kuimarika.
“Mechi hizi za Kombe la Dunia unatakiwa kushinda nyumbani zote, mipango ambayo kwetu bado inakwenda vizuri. Tukiwafunga Morocco kwao tutazidi kuimarika. Tunajua mechi itakuwa ngumu, nasi tumejipanga kwa hilo tukijua Morocco wanacheza nyumbani na watakuwa katika shinikizo kubwa kutoka kwa mashabiki wao,” alisema Kim aliyeanza kuinoa Stars tangu Mei mwaka jana.

Atachezesha washambuliaji wangapi mwisho? Jibu la Kim katika swali hilo ni kuwa timu iko kwa ajili ya kutengeneza nafasi za kufunga, hivyo washambuliaji inabaki kuwa suala la namba tu.
Lakini akaongeza kuwa aina yao ya kushambulia itategemea na staili ya uchezaji ya wapinzani wao.
Kwa hapa Marrakech mechi hiyo imekuwa haizungumzwi mara kwa mara, na kubwa ni kuwa Wamorocco wengi wanaamini kuwa timu yao ambayo hadi sasa ina pointi mbili haina nafasi ya kusonga mbele katika hatua inayofuata ya michuano hiyo. Kikosi kinachotarajia kuanza cha Stars huenda kikapangwa hivi; Juma Kaseja, Erasto Nyoni, Shomari Kapombe, Aggrey Morris, Kelvin Yondani, Frank Domayo, Mrisho Ngasa, Salum Abubakar, Thomas Ulimwengu, Amri Kiemba na Mbwana Samata.

No comments:

Post a Comment