tuwasiliane

Thursday, May 30, 2013

MWENYEKITI WA JUMUIYA YA VIJANA CUF TAIFA(JUVICUF) MHE. KATANI A. KATANI AMEKAMATWA NA ANASHIKILIWA NA POLISI JIJINI DSM

Kwa mujibu wa naibu katibu mkuu wa CUF bara bwana Julius Mtatiro kuwa
Mhe. Katani alipigiwa simu leo mchana na kutakiwa kuripoti CENTRAL POLICE. Alisindikizwa na baadhi ya viongozi na mwanasheria. Walipofika aliwekwa chini ya Ulinzi na akajulishwa kuwa angesafirishwa leo hii kupelekwa Mtwara ambako anapaswa kujibu tuhuma zinazomkabili.

 Yeye(Mtatiro)na Mwenyekiti Taifa (Prof. Lipumba) tumekwenda MAKAO MAKUU YA JESHI LA POLISI na kukafanya kikao kifupi na IGP Mwema na DCI Manumba juu ya masuala hayo. Tumekubaliana kuwa atasindikizwa na makachero kesho asubuhi kuelekea Mtwara kwa ndege na kisha taratibu za kisheria zitaendelea hukohuko.

Wanasheria na mawakili wetu na viongozi pia watakuwa Mtwara kujua suala hili litakwendaa vipi. Kabla Mhe. Katani hajakamatwa leo, amewahi kuhojiwa mara kadhaa na makachero wa polisi Mtwara na DSM kabla kabisa ya vurugu za hivi majuzi na mara zote alionesha ushirikiano mkubwa.

Tumejulishwa kuwa kati ya watu wanaoweza kukamatwa baada ya Mhe. Katani ni pamoja na Mhe. Selemani Bungara(MB) - Kilwa Kaskazini pamoja na viongozi kadhaa waandamizi. Tumewajulisha viongozi wetu wasiwe na hofu, wasiondoke makwao na ikiwezekana wajipeleke polisi wakijua wanatafutwa.

Cha kushangaza ni kuwa, viongozi hawa wote wanaokamatwa, mara kadhaa wamewahi kuendesha mikutano mikubwa na halali iliyolindwa na polisi ambapo walipinga mpango wa serikali kusafirisha gesi kwenda DSM bila kuhakikisha maslahi ya Mikoa ambayo gesi imevumbuliwa. Na haya waliyafanya kwa kujenga hoja za kawaida kabisa majukwaani, zaidi ya hapo hawajawahi kuhusika na masuala ya uchochezi.

Tumemweleza IGP na DCI kuwa wawaambie serikali kuwa wao serikali ndo wamechochea vurugu za Mtwara kwani JK mwenyewe aliwaahidi wananchi wa Mtwara masuala kadhaa kuhusu gesi na hadi leo hayajatekelezwa. Tumewaeleza waziwazi kuwa suala la gesi siyo jepesi sana na halitamalizwa kwa kuwakamata wanasiasa wasio na hatia.

Suala la gesi litamalizika kwa salama ikiwa serikali itafungua milango ya mazungumzo na maelewano na wananchi inakotolewa ikiwa ni pamoja na juhudi kubwa za kuwaelimisha wananchi wa mikoa husika na kuwatengenezea miradi mingi yenye tija ambayo italeta ajira na kupanua uchumi wa wananchi wa mikoa ya kusini ili waondokane na umasikini wa kutupwa.

Serikali iache kiburi ambacho hakina mantiki kwa sasa, ifanye kazi kubwa ya kulitatua suala hili kwa busara. Kuwakamata viongozi wetu siyo suluhisho, tutaendelea kutoa maoni na mapendekezo yetu kama chama bila kificho chochote hata kama watatukamata wote. Serikali itatue kiini cha tatizo, iache kutibu matokeo.

Mwisho wa siku ukweli utasimama, Wananchi wa Lindi na Mtwara wasikilizwe na tuache ubabe usio na maana.

Ndiyo, gesi ilinufaishe taifa, lakini tuwe na utaratibu maalum, tuwe na sera ya gesi na ikiwezekana tuboreshe sheria zetu ili kufanya rasilimali za taifa zilinufaishe taifa pamoja na wakazi wa maeneo ambako rasilimali imepatikana.

No comments:

Post a Comment